Watu 18 wauawa katika shambulio la makombora la Marekani dhidi ya Iran

Chanzo cha picha, Getty Images
Waziri wa Afya wa Iran, Mohammad Reza Zafarghandi, ametangaza kuwa watu 18 wameuawa na wengine 108 wamejeruhiwa katika mashambulizi yaliyofanyika katika majimbo mbalimbali ya Iran usiku wa kuamkia leo.
Hili ni miongoni mwa mashambulizi mabaya zaidi yaliyofanywa na Marekani tangu vita vya siku 40 kuanza.
Milima ya Sirik ni miongoni mwa maeneo yaliyoathiriwa na mashambulizi ya Marekani.
Maafisa wa Iran wamesema watu wanne, akiwemo mwanamke na mtoto waliokuwa wakihudhuria harusi, waliuawa na wengine 65 kujeruhiwa katika mashambulizi hayo.
Pejman Shahrokhi, Rais wa Chuo Kikuu cha Sayansi za Tiba cha Hormozgan, amesema majeruhi sita katika tukio hilo lililotokea katika Milima ya Sirik wako katika hali mahututi na wamelazwa katika kitengo cha wagonjwa mahututi (ICU), huku wengine 26 wakiwa katika wodi ya upasuaji.
Akijibu swali la BBC Persian, msemaji wa CENTCOM, Kapteni Tim Hawkins, hakukanusha shambulio hilo, akisema alikuwa anafahamu taarifa hizo.
Alisisitiza kuwa vikosi vya Marekani havilengi raia. Katika jimbo la Khuzestan, watu saba waliripotiwa kuuawa na wengine wanane kujeruhiwa katika mashambulizi yaliyofanyika maeneo ya Ahvaz na Aghajari.
Angalau mmoja wa waliouawa ametambuliwa kuwa mwanachama wa kikosi cha usalama.
Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu nchini Iran (IRGC) pia limethibitisha kuwa wanajeshi wake wanne wa kikosi cha anga waliuawa katika jimbo la Kermanshah.
Taarifa nyingine zinasema wapiganaji watatu wa Basij waliuawa baada ya shambulio la Marekani katika Kisiwa cha Lavan.











